Pekua/search

Thursday, September 24, 2009

TUJADILI MIHTASARI MIPYA YA MAFUNZO YA UALIMU 2009

Ndg wadau

Wizara ya Elimu na mafunzo ya Ufundi wiki iliyopita ilitoa miongozo mipya [Sylabus] kwa ajili ya kufundishia katika vyuo vya Ualimu kwa ngazi zote za cheti na stashahada.Kupata miongozo hiyo Bonyeza HAPA

Na John Malata

Chanzo: Wanazuoni yahoo groups

Adam alichangia ifuatavyo:

Amani kwako John na wanazuoni.

Shukrani kwa kutupa ujumbe huu muhimu. hata hivyo nanalo dukuduku, ninaomba wanazuoni weledi mnisaidie, mkiweza.

Hii mihtasari iliyotolewa inahusiana vipi na Sera mpya ya Elimu na Mafunzo 2009, ambayo ndiyo kwanza 'inaandaliwa' ?

Je kimantiki haikupaswa sera mpya itangulie kuwepo ndipo mihtasari ambayo kimsingi ni miongozo inayoelekeza utakelezaji ambao utawezesha kufikiwa kwa matamko ya sera kisha kufikiwa kwa malengo ya sera husika na hatimaye malengo makuu ya taifa, Dira ya Maendeleo ya taifa?

Kwa ufahamu wangu mdogo Sera inatoa mwongozo wa jumla na kisha mipango mbali mbali na mihtasari kama hiyo ndiyo inaelekeza kinagaubaga (kitaalamu) namna ya kutekeleza. Baada ya kuyazingatia maelekezo yaliyomo kwenye sera ndipo miongozo mbali mbali, ikiwemo mihtasari inapaswa kuandaliwa. Sasa kama hivyo ndivyo kwanini mihtasari mipya ya mafunzo ya ualimu (ambayo kwa kiasi kikubwa ni muhimili muhimu wa kutekeleza sera) inatolewa mapema? tutakuwa na uhakika gani kwamba mihtasari hiyo haijafuata malekezo ya sera ya zamani? na kama sivyo, je ndiyo kusema sera mpya inayojadiliwa sasa tayari imepitiswa na kinachofanyika hivi sasa (kupata maoni ya wadau) ni usanii tu?

Je hauwezi huu kuwa ufisadi, tena mbaya kuliko aina nyingine za ufisadi? Sera haijatoka, mihtsari inatolewa, kwa haraka gani? Kwa faida ya nani? nisaidie jamani!!! Huenda hili sio kosa dogo. Kama walimu wakiandaliwa tofauti na maelekezo ya sera, je si hatari iliyoje?

Nawasilisha

5 comments:

Anonymous September 24, 2009 at 2:57 AM  

Kuna vitu ambavyo tunaweza tukawalaumu hawa watunga sera lakinni kwa kiasi fulani wamefanya maboresho ngazi ya stashahada.Stashahada walikuwa wanasoma mwaka mmoja chuoni ,muda unaobaki mazozi ya muda mrefu ya kufundisha,hii haikuwa nzuri lakini kwa sasa watakuwa na wiki nane za mazoezi kwa miaka miwili hii inatia moyo.
Matatizo nayaona katika kiwango cha ngazi yya cheti darajala tatu A.Hawa wameongezewa masomo wakati huohuo kuna masomo ambayo yamefutwa hii itafanya baadhi ya masomo wasome kwa kifupi sana hasa yale ya ualimu.
Dosari nyingine ni kufuta michepuo kwa walimu tarajali hawa.kwa sasa wanatakiwa wasome sayansi na lugha,hii haijalishi kama mwalimu tarajali huyu alisoma sayansi au la!Hapa tunatarajia kuzalisha walimu vihiyo sabu iliyotumika ni kuwa hawatashindwa kufundisha hesabu wala sayansi kwa shule za msingi.
Kuhusu muhtasari huu kuanza kutumika kabla ya sera mpya ya elimu kuna usanii na ujasiri hapa!Ujasiri ninaouona ni kubobesha elimu kwa walimu wa sekondari.
Usanii nchi hii ni kawaida yetu watu hawa walikuwa wanataka kula na kweli wamekula nahili walikuwa wanalijua kwani walikutana kupanga na walikubaliana kubadilisha muhtasari kabla ya sera mpya ya elimu.
Yawezekana sera hii impya ni danganyatoto.

zenga September 25, 2009 at 12:09 AM  

naomba nikutoe wasiwasi ndugu yangu.nachangia nikiwa kama mdau wa elimu na nimejaribu kulinganisha sera ya zamani na sera mpya ya elimu.
Muhtasari wa vyuo vya elimu kuanza kutumika mapema kabla ya sera ya elimu sio tatizo kwani imeboreshwa zaidi.Wanafunzi walimu wanaandaliwa katika mbinu na maudhui.
ukiangali kwa makini jambo hili lina faid a kwa taifa kwani walimu waaaaaaaanaoandaliwa sasa wanapikwa zaidi hivyo ni vema hawa walioingia mwaka huu wakaanza na hayo mabadiliko madogo tukiendelea kusubiri sera mpya ambayo watakutana nayo watakapokuwa kazini.

Adam September 25, 2009 at 1:10 AM  

Nakushukuru sana ndugu Zenga kwa mchango wako. Pia nakushukuru zaidi kwa kujaribu kunitoa wasiwasi.

Hoja niliyokuwa nikijaribu kuiibua iko katika mantiki ya uhusiano wa uboreshaji wa Mihtasari hiyo na sera ya elimu na mafunzo.

Kwanza ndugu mdau mwenzangu wa elimu tukubaliane kwamba waalimu hawakutani na sera kama sera vyuoni au kazini kama usemavyo.Wanakutana au niseme wanapaswa kukutana na tafsiri ya sera iliyowekwa kiutekelezaji.Ama nifafanue kuwa wanakutana na miongozo ya utekelezaji wa sera hizo, mkubwa ukiwa ni mihtasari ya masomo. Ndiyo kusema tunakutana na sera kwa maana ya sheria na kanuni za utekelezaji wa sera husika. kwa hiyo miongozo kama vile mihtasari ndiyo ' sera' yenyewe ikiwa kazini.

Hapa namaanisha kwamba mihtasari ya mafunzo ya ualimu, na ngazi nyingine yoyote ya elimu, haina budi kuakisi sera ya elimu na mafunzo. Sera hiyo haina budi kuakisi falsafa ya elimu ya taifa ambayo nayo inaakisi dira ya maendeleo ya nchi,n.k.

Unaposema hivi sasa mafunzo ya ualimu yanatolewa vizuri zaidi UNAPIMA KWA MISINGI IPI? Je itakuwa vipi ikiwa itapingana na sera ya elimu na mafunzo, mathalan. Lakini zaidi sana muhimu ni kulikuwa na haraka gani na ya nini ya kutoa mihtasari wakati sera iko hatua za mwisho kutolewa?
Na kama tutaona kwamba mihtsari yaweza kwenda kimpango wake, hivi SERA ni nini? Na inawekwa ili iongoze nini kwa manufaa ya nani??
nachangia.

Anonymous September 25, 2009 at 4:56 AM  

Adam,napata faraja sana kutambua kuwa uliiva hasa katika swala la mitaala ulipokuwa shule.Inatia kinyaa kuona watu wenye visomo vilivyobobea wanapofanya mambo kama majuha.

Siamini kama kweli wamelifanya hili kwa bahati mbaya.Kutoa miongozo kabla ya resa! Sijapata ona.Wameshindwa kuhusianisha Siasa ya nchi,Philosofia ya elimu ya nchi,Dira ya maendeleo ya nchi,seara na mihutasari.

Ni kweli kuwa kuna maboresho yamefanyika fine !Lakini je hayo maboresho yanaakisi sera ipi? tunayoboresha au ile ya zamani?

Adamu na wadau wengine.Sera ya mafunzo ya 1995 ilipotoka mihutasari ya ualimu ilitoka baada ya miaka nane! yaani 2003.Anyway sitaki niende mbali sana.Mimi nipo jikoni kama sio ktk mlango wa jiko.(Teacher education )Syllabus ndio hiyo imebadilika kuanzia primary-2005,sekondari-2007 na vyuo-2009.Ikiwa kanuni zitafuatwa basi ni matarajio yangu kuwa mitaala itabadilika tena muda sio mrefu ili kukidhi haja ya sera mpya itayokuja.

Poleni wadanganyika!!!

Adam September 25, 2009 at 5:52 AM  

Ewe mdanganyika mwenzetu shukrani kwa maelezo mazuri. Lakini je tutakuwa wadanganyika mpaka lini? Kwa hakika vitu vingine wala havihitaji uzamivu wala ubobezi wa kihivyo, kama hili la mama (SERA) kuzaa mtoto (Sheria, kanuni, na miongozo - MIHTASARI!!!

Wacha nikupeni hadithi ya kweli (kama kuna kitu nimesoma kwa muda mrefu ni fasihi - kwa hiyo nisamehewe!!!)

Siku moja miaka ya mwanzoni mwa 2000 nilisafiri kwa basi la SUMRY kutoka Sumbawanga kuelekea MBEYA. Ilikuwa msimu wa mvua nyingi. huko njiani ilikuwa ni kushoto kulia sendemaaa, roho mkononi, mshike mshike.

Kilichotokea ni kwamba barabara ilikuwa imemwagiwa kifusi siku chache tu, kwa hiyo iligeuka dimbwi la tope!!

Bahati nzuri nilikuwa na mwalimu wangu wa enzi za sekondari bwana Sirinu (Mungu amrehemu). kwa vile mtoto kwa baba hakui, nikamuuliza mwalimu inakuwaje hawa makandarasi wanapewa kazi ya kujaza tope barabarani kipindi kama hiki? Kwani wao wageni 'yerusalemu, hata hawajui kuwa kipindi hiki ni cha mvua? Mwalimu akaniambia kuwa si tu kwamba sio wageni lakini pia wahandisi wa mamlaka husika ni WASOMI WAZURI SANA.

Nikauliza sasa kwanini wanafanya hivi? Hawajui kwamba wanapoteza pesa za walipa kodi bure? Kwani hawawezi kusubiri hata mvua ikaisha? jibu lake lilinishibisha na nikajiona mjinga mimi.Alisema;

'Bwana mdogo, sasa kama hela zimekuja kipindi hiki unataka wasubiri mpaka kiangazi, kwani wanauhakika kuwa watakuwepo kwenye nafasi walizopo mpaka hicho kiangazi chako kifike? Kwani pesa za walipa kodi zikipotea, si zinapotelea mifukoni mwao? Kwanini wajali?'

Majibu ya mwalimu wangu yule mpendwa yalinifungua macho. na ninadhani yanaleza kwa undani msukumo wa utendaji wetu katika idara na sekta mbali mbali. Hatusukumwi na ubora, bali tumbo street; umimi.

Kama ndugu Zenga alivyobainisha, kweli uzuri wa hapa na pale unaweza kuonekana, lakini ni uziri wa mkakasi, ndani kipande cha mti. Uzuri wa barabara zinazotengenezwa kwa kumwaga na kushindilia kifusi kipindi cha masika, hatari yake ni kubomolewa na mvua na kugeuzwa makorongo!! Sawia, uzuri wowote unaweza kuwepo kwenye mihtasari iliyoandaliwa kwa timing, kuhofia mwaka wa uchaguzi mwakani, na kwamba baadhi ya wataalamu hawana uhakika iwapo baraza jipya likingia madarakani kama watabakishwa kwenye nyadhifa ambazo huenda wamepewa kiswahiba, hatari yake ni kuwepo kwa mfumo usiosaidia kulipeleka taifa kwenye tija na ufanisi.

Mafunzo ya ualimu kwa mtazamo wangu mimi ni muhimu sana katika kutekeleza malengo ya kisera ya kuboresha elimu katika ngazi zote ili kufikia malengo ya dira ya maendeleo ya taifa ambayo kwa kunukuu ni "(Tanzania) Be a nation with high quality of education at all levels; a nation which produces the quantity and quality of educated people sufficiently equipped with the requisite knowledge to solve the society's problems, meet the challenges of development and attain competitiveness at regional and global levels," naam ndivyo isemavyo dira 2025.

Tuendelee, hata kama wahenga walitoa kejeli kuwa ada ya mja ni kunena; Bora tu tunene maana kunena ni karibu sana na kutenda; hakika kuandika ni kutenda pia.

SUBSCRIBE- Andika email yako hapa utumiwe habari mpya

Enter your email address:

Delivered by FeedBurner

  © Blogger templates 'Neuronic' by Ourblogtemplates.com 2008 modified by Subi nukta77

Go Back to TOP