Pekua/search

Saturday, November 30, 2013

Upuuzi wetu kuhusu mgogoro wa CHADEMA



Upuuzi wetu kuhusu mgogoro wa CHADEMA

Wapambe na kina 'nitoke vipi' ni balaa kuliko hatari yenyewe

 
Mbowe, Slaa na Kabwe
Tutakuwa wapuuzi kutarajia kwamba chama cha siasa cha ‘ukombozi’ kama CHADEMA kistawi pasipo migogoro na migongano! Tutakuwa hatuwatendei haki viongozi wa chama hicho na zaidi kutojitenddea haki sisi wenyewe maana tutakuwa tukiishi katika ulimwengu wa kufikirika, ruya ya mchana.

Hata hivyo nadhani ni sahihi kwa wafuasi na au mashabiki wa chama hicho kutarajia mikakati madhubuti ya chama katika kuzuia au kupunguza migogoro na migongano, hususani ile isiyo ya lazima. Ni vema na haki kwa wanachama, wafuasi, mashabiki na wapenda demokrasia kuweka matarajio makubwa kabisa kwa chama kama CHADEMA kuwepo kwa mbinu zenye makali za chama husika katika kutanzua migogoro. Hili ni muhimu maana litaakisi matarajio mapana kwamba iwapo chama hicho kitachukua hatamu za dola, kitafanya vizuri zaidi ya watawala na viongozi waliopo madarakani.

Hapana budi chama chenye kujipambanua kuwa cha mbadala, kikawa na hazina ya busara na weledi unaotakiwa kuibadili  tufani inapoibuka na kuwa utulivu.
 
Kabwe na Mbowe: Kanyaga twende
Hayo yote, mbinu, hekima na weledi yanahitajika sio kwa chama pekee kama chombo bali pia wale wanaojitutua kutaka kushika hatamu za uongozi wa taasisi yoyote kuanzia chama husika hadi taifa. Hapana budi waonyeshe pasipo shaka kwamba wanawazidi wengine kwa mbinu, na busara katika kushughulikia matatizo.

Na busara ya zamani kabisa ya Mfalme Suleimani inatuelekeza kwamba, ni upuuzi usiokifani kuendekeza, “tukose wote”!

CHADEMA na wahusika wote kwenye mtafaruku huu ni lazima wawashinde wapambe na wale kina nitoke vipi! Zitto anao mtihani katika hili, Uongozi wa CHADEMA kwa ujumla unayo changamoto pia. Ni lazima kuwashinda wale wote wanaotaka kujinufaisha na mgogoro huu iwe kwa mali au kutaka umaarufu tu. Wapambe ni hatari kuliko hatari yenyewe. 

Natumaini CHADEMA kitashinda mtihani huu waliojitungia wenyewe.  Nina matumaini makubwa kitaimarika sana. Upepo mkali husaidia sana kujua nakutofautisha matawi imara na yale dhaifu yapukutikayo!
Kila lenye heri tumaini la watanzania! 
Mkumbo na Kabwe

Wednesday, November 27, 2013

Kudorora kwa Elimu nchini- Tatizo ni Rais Kikwete au Watanzania?



Kudorora kwa Elimu nchini- Tatizo ni Rais Kikwete na Watanzania?
 
Shukuru Kawambwa, Waziri- WEMU
Je Mhe. Rais, ametoa baraka kwa wateule wake (Waziri/Naibu Waziri kwa upande mmoja na Katibu Mkuu wa Wizara) Kutenda kazi kimzahamzaha? SIAMINI!

Inashangaza kuona Katibu MKuu wa Wizara ya Elimu (WEMU) anatangazia umma kuwa muundo wa upangaji wa madaraja na madaraja yenyewe vimebadilika, kisha siku inayofuata Naibu waziri wa wizara hiyo hiyo anapinga habari hiyo mchana kweupe!!! Inashangaza.

Lakini inashangaza na kusikitisha zaidi kuona kwamba inakuwa siku ya kwanza, wiki ya kwanza na ya pili na ya tatu nap engine mwezi....Watu hawa hawajawajibika na hata Mamlaka ya Uteuzi (RAIS) hajawawajibisha.

Naibu waziri WEMU, Mlugo
Inatisha kabisa kuona jinsi tulivyojikalia kimya kama watanzania utadhani hakuna kilichotokea! Tusipoenda barabarani kuhusu hili ni jambo gani litatupeleka huko? Hapa suala ni zaidi ya kuwepo au kutokuwepo kwa hiyo div 5. Suala ni pana zaidi maana linahusu utendaji wa wizara hii muhimu. Maskini sisi!

Pongezi zangu za dhati kwa Nape Nnauye, katibu mwenezi wa CCM kwa kulisema hili wazi wazi kuwa Waziri wa Elimu, with due respect, kazi imemshinda.  Haiwezekani hata kidogo viongozi wakuu kabisa wa wizara moja wakasema mambo yanayokinzana ndani ya wiki moja! Mawasiliano yao yakoje? Na kama ni mabaya, hiyo sio dalili bali ni KUSHINDWA KAZI KABISA!

Bila elimu bora ya ya uhakika Tanzania itakuwa taifa la namna gani? Na bila ya umakini na weledi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi  elimu bora itapatikanaje? Inakeraaaaaaa! Inakarahishaaaa!
Katibu Mkuu WEMU, Prof Sifuni Mchome na Kamishna wa Elimu, Prof. Eustella Bhalalusesa

Thursday, November 14, 2013

Mauaji ya Dkt. Mvungi- Jambazi Sugu hili hapa



 Mauaji ya Dkt. Sengondo Mvungi- Jambazi Sugu  hili hapa

Suleiman Kova, Kamanda Kanda Maalum Dar es Salaam
 Jambazi sugu hili hapa, mwaliona?
Limeshiriki kumuua dakta wetu Sengondo Mvungi, nani atapona?
Huenda na wengine kama Jwani, nani atakana?
Na kujeruhi wengine kama Dkt. Ulimboka, inawezekana!
Ni jambazi sugu hili, licheki lilivyo pozi, si mwaliona?
Ni jambazi sugu hili lilipohojiwa limekiri, bila kujibana!
Na limekiri haraka kweli kweli,pasikubishana!
Limejitolea kutuonesha na bastola ya dakta Mvungi, hakuna kusigana!
Ndiyo, ni lijambazi sugu limekamatwa likiangalia RUNINGA!
Jinale Ngosha, John Mayunga!

Jamani lijembawazi hili si mmeliona?
Mmelitazama vizuri lakini?
Hilo hapo msijeleta visingizio,
mkadhani ni njama. Ni ujambazi!

Jamani hizi sio ngojera za kuburudisha tu, sawa?
Bali ni TAMthilia (sema CHUNGU) iliyosukwa mahsusi, haina dawa!
Msijesema mlizisikia kwa ulimboka na Yule Mulundi, Mkenya, si ilikuwa powa?
Msijesema ni zile zile, msijifanye mmezizoea, mtabishiwa!
Hili ni lijambazi sugu, si  lilifungwa?,
Limetoka jela, au mwadhani  mahsusi limetolewa?
Ndiyo, hata kama bado halijatoka, si vibaka walitumwa?.
Vibaka kwa kawaida hawahitaji mali ama fedha, Mwaelewa?
Hutaka laptop na nyaraka, si ni vibaraka wenye viraka?

Shenzi zao vibaka wanaopenda kudaka laptop!
Pumbavu zao vibaka hawa wanaohitaji nyaraka nyeti

Oh no! na jambazi sugu lilikuwepo.
Li John Mayunga, Ngosha si la depo!
Tena na baruti zilikuwepo
Hata haya yatapita kama upepo.
Viva Kamanda Kova! Kazi nzuri.
Endelea mpaka mwisho.
Buriani Msomi Mweledi Sengondo Mvungi.
Kwaherini.
Dkt.Sengondo Mvungi, Pumzika kwa Amani

Wednesday, November 13, 2013

MOURNING DR. Sengondo Mvungi NO MORE



Sikulilii Tena Dkt Sengondo Mvungi.



Najililia Mwenyewe na Tanzania hii.



Injili ya Luka 23:




28 Yesu akawageukia, akasema, "Enyi kina mama wa Yerusalemu! Msinililie mimi, ila lieni kwa ajili yenu wenyewe na kwa ajili ya watoto wenu. ...



29 Maana, hakika siku zitakuja ambapo watasema: `Heri yao wale walio tasa, ambao hawakupata kuzaa wala kunyonyesha watoto!`



31 Kwa maana, kama watu wanautendea mti mbichi namna hiyo, itakuwaje kwa mti mkavu?"



Maandiko yameweka wazi na bayana kabisa. Sina sababu ya kulia tena. Jana nimekulilia kwa sababu ya ujinga. Nililisahau neno hili. 

Mwenzetu Mvungi alikuwa na heri. alipata nafasi ya kujililia mwenyewe. Kumbukumbu zinaonyesha alimwaga chozi hadharani, aliposoma shairi la kumuaga Prof. Jwani Mwaikusa, ambaye naye aliondoshwa kwa mwendo wa aina hii. Alijililia msomi huyu,maana hakujua nani ATAFUATA BAADA YA JWANI. 


Mkumbushe chozi hili la Nkurumah, Jwani Mwaikusa.
Iwapo kuna kuonana mpe salaam Nyerere,na Kambona, na Kombe, na Danny Mwakiteleko na wengine na wote wengi!!!




Nenda nenda kamanda. 
Tulikuita Kichwa,
Dict alikuita Rodney,
Happy Katabazi, 'Rais Mdhulumiwa',
Sikukufahamu sana. 
Vikao viwili vitatu vya kimakakati,
Vimebakisha kumbukumbu mbichi nafsini. 
Nenda tu Mvungi nenda.



Mwaondoka wenye kunena,
Wanaondoka wenye kunyamaa,
Ole wangu!!


Tulijua yako thamani,
Tulielewa u mtu makini,
Sikika wanasikika, hawaeleweki
"Huduma za Matibabu ya dharura si Anasa", tunafanya kusudi. 

Tulishindwa kukulinda,
Tumeshindwa kukutibu kwa dharula.



SUBSCRIBE- Andika email yako hapa utumiwe habari mpya

Enter your email address:

Delivered by FeedBurner

  © Blogger templates 'Neuronic' by Ourblogtemplates.com 2008 modified by Subi nukta77

Go Back to TOP