Pekua/search

Monday, October 25, 2010

Mambo 10 unayotakiwa kujua kuhusu Kura yako

Mambo 10 unayotakiwa kujua kuhusu Kura yako

by Mimi Mwanakijiji on Tuesday, October 26, 2010 at 5:29am
MAMBO AMBAYO UNATAKIWA KUJUA KUHUSU KURA YAKO:Na. M. M. Mwanakijiji

Kura yako ina nguvu gani na kwanini?

1. Kura yako ndiyo lugha pekee ambayo wanasiasa wanaielewa. Wanasiasa wote duniani wanaweza kuwa wabishi na wenye kelele sana lakini ni kura tu ndiyo inaweza kuwalazimisha kusikiliza. Kama unataka kumwambia mwanasiasa akusikie? Piga kura!

2. Kura yako ni silaha pekee katika demokrasia ya kuwaadhibu wanasiasa wabovu na viongozi uchwara. Katika demokrasia wananchi waliochoshwa hawahitaji bunduki wala mapanga kuonesha hasira yao, wanahitaji karatasi ya kura na kutoa kipigo chao kwenye sanduku la kura! Ndio maana tunaita “kupiga kura”!

3. Kura yako ni siri yako. Hakuna mtu anajua umepigaje au utapigaje kura hata kama anajua wewe ni mwanachama wa chama gani. Kama siri nyingine za mioyo njia pekee ya mtu mwingine kujua ulivyopiga kura ni kwa wewe kumwambia, usipomwambia hawezi kujua. Hakuna Polisi, Idara au chombo chochote cha usalama kinaweza kujua ulivyopiga kura! - Piga Kura

4. Kura yako ndio utekelezaji wa uamuzi wako. Mtu kabla hajapiga kura ni lazima afanye uamuzi kwanza ni mgombea gani anamtaka na kwanini na akishafikia uamuzi huo basi anaingia kwenye chumba cha kupigia kura na kuutekeleza uamuzi huo. Bila kupima uamuzi wako utapata shida kupiga kura, amua kwanza, halafu piga kura!

5. Kura yako si deni kwa mtu au chama chochote. Pamoja na kuwashangilia wagombea au kuonesha kupendezwa na hoja zao hayo yote hayakufanyi ujihisi unadaiwa nao. Kura ni haki yako wewe siyo haki yao wao. Hivyo, una haki ya kumpa mtu yeyote kura hata kama si wa chama chako bila kujisikia umemnyima mtu haki yake. Kura ni haki yako wewe!

6. Kura yako yaweza kwenda kwa mtu yeyote au chama chochote bila kukufanya ujisikie umsaliti. Utakapoingia kwenye chumba cha kura una haki ya kubadilisha kura yako kwa kadiri ya dhamira yako. Ukiwa na wasiwasi kuhusu kumpigia kura mtu hasa unayemtaka kwa kuogopa kuwa wanaweza kukujua soma namba  (3). Piga kura kwa kufuata dhamira!

7. Kura yako ina matokeo kwa vizazi vijavyo siyo kwa leo tu. Usipige kura kwa kuangalia furaha ya leo au kukidhi mahitaji ya leo tu, kura utakayopiga itaamua nani apange mipango na kusimamia mipango kwa miaka mitano ijayo na mingine inayoweza kuvuka vizazi. Hivyo, usipige kura kwa kuridhisha hisia za leo, fikiria kizazi kijacho kitanufaika na uamuzi wako?

8. Kura yako inapoombwa na wagombea wanachogombea ni ajira kutoka kwako. Wewe ndiye muajiri wa wanasiasa wote kuanzia Rais hadi diwani. Hawana haki na kura yako kama vile mfanyakazi hana haki na mali ya bwana wake. Ndio maana wanapita kuomba kura yaani ajira. Ni lazima ujiulize je kama mtu anaoomba kibarua kwako utampa tu bila kuangalia kama ataweza kufanya kazi na unaweza umuamini? Hivyo, baada ya kuwasikiliza waomba kazi waliopiga kila sehemu je uko tayari kuwaajiri wakufanyie kazi ya kuliongoza taifa lako?

9. Kura yako ndiyo huduma zote za jamii unazozitaka. Kwa vile kura yako ndiyo inaamua nani anaingia madarakani na kupanga nini na kutekeleza vipi basi kura yako ndiyo itaamua watoto wako watasoma katika shule gani, mfumo wa utawala utakuwaje, jeshi la polisi linafanyaje kazi n.k Hivyo, kura yako ndiyo barabara, maji, elimu, utawala, n.k Piga kura ukijua unataka upatiwe nini na nani?

10. Kura yako ni dhamiri yako. Kila mwanadamu anayo dhamira ndani yake yaani ile sauti ya ndani inayotufanya tukatae vitu vibaya na kuvipenda vizuri, ile sauti inayotuonya tunapofanya vibaya na kutupongeza tunapofanya vizuri. Ni ile sauti ya kimya ndani ya mioyo yetu inasimama kama shahidi wa maamuzi na matendo yetu. Dhamiri hii katika siasa inaoneshwa katika kupiga kura. Unapoenda kupiga kura hakikisha umepima mambo yote yanahuusu wagombea na ajenda zao na mwisho fuata dhamira yako. Usipoisikiliza dhamiri yako utaishi na majuto, usiishi na majuto!

Hivyo basi, tumia haki yako ya kupiga kura kumchagua mgombea ambaye unajua atafaa kuliongoza taifa kwa miaka mitano ijayo. USIOGOPE, USIBABAISHWE NA KAMWE USITISHWE ATI USIPIGE KURA! Weka miadi na historia, piga kura!

0 comments:

SUBSCRIBE- Andika email yako hapa utumiwe habari mpya

Enter your email address:

Delivered by FeedBurner

  © Blogger templates 'Neuronic' by Ourblogtemplates.com 2008 modified by Subi nukta77

Go Back to TOP