Pekua/search

Tuesday, April 16, 2013

KUPANDA KWA BEI ZA NAULI NA ATHARI ZAKE KWA WANANCHI WENYE KIPATO CHA CHINI



Kupandishwa kwa gharama za usafiri kumekuwa na mapokeo hasi kwa baadhi ya wadau jijini Mwanza, hasa ukizingatia gharama za maisha kuwa juu, zaidi kwa watu wenye kipato cha chini. 

Wakiongea na mwandishi wa makala haya kwa nyakati tofauti tofauti, juu ya ni kwa jinsi gani wamepokea kauli iliyotolewa na mamlaka ya uthibiti wa usafiri wa majini na nchi kavu (SUMATRA) juu ya  kupandishwa kwa nauli, wadau tofauti tofauti walikuwa na maoni mbalimbali juu ya suala hilo 

Bwana Gudluck John, mtumishi katika sekta ya umma,  anasema, “nilipokea taarifa hiyo kwa mstuko sana ukilinganisha na hali ya maisha kuwa ngumu. Kiwango kilichopandishwa ni kikubwa sana ukizingatia ukweli kuwa hali hiyo itapandisha gharama  za maisha wakati misharaha haipandishwi.”

“Kwa sasa nitatakiwa kutumia TSH 800/= kwa siku kwa ajili ya usafiri, gharama ambayo kwa mweizi itakuwa takribani TSH 24,000/=. Nikiongeza na nauli ya watoto wangu watatu, ambayo itakuwa takribani TSH  37,000/=, kwa mwezi nitakuwa natumia  zaidi yaTSe3H 61,000/=; gharama ambazo ni kubwa sana ikiwa mshahara utabaki kuwa ule ule ambao nilikuwa natumia nauli ya takribani 32,550/= kwa mwezi,” Bwana Gudluck anafafanua. 

Bibi Angela Willy, mkazi wa Butimba na mtumishi katika sekta binafsi, anasema kuwa hofu yake kubwa ipo kwenye upandaji wa bei za vyakula kutokana na gharama za usafirishaji. “Bajeti yangu kwa ajili ya chakula itaongezeka kulingana na bei ya vyakula itakavyopanda. Jambo ambalo litafanya maisha kuwa magumu kwani mshahara huo huo niupatao ndio  utatakiwa kugharamia gharama hizo”, anasema Bi Angela. 

“Serikali pamoja na waajiri katika mashirika yasiyo ya kiserikali  watufikirie wafanyakazi, kutokana na gharama za maisha kupanda, kwa kutuongezea mishahara ili tuweze kumudu hali hii” anashauri  Bi Angel.

Hata hivyo, kwa kuhusu suala la upandaji wa bei za vyakula, imeelezwa kuwa kupanda huko kwa nauli hakutoathiri bei za vyakula katika masoko ya bidhaa hizo jijini kutokana na msimu wenyewe kuwa ni wa mavuno.   

Athuman Kalinga ni msafirishaji  wa bidhaa mbalimbali za vyakula kutoka Bukoba na kuzileta katika soko kuu jijini humo anasema kuwa, pamoja na kupanda kwa bei za nauli yeye na wafanyabiashara wengine hawatoathirika kiasi cha wao kupandishiwa gharama za usafirishaji wa bidhaa hizo kutokana na sababu kuwa usafiri mkubwa wanaotumia ni kwa njia ya meli na kuwa gharama za usafirishaji zinaendana na kiasi cha bidhaa zinazosafirishwa.

“Asilimia kubwa ya mchele unaouzwa katika maeneo mbalimbali ya jiji hili ni kutoka Mwanza na shinyanga ambapo husafirishwa kwa njia ya marori lakini maharagwe na mahindi hutolewa mkoani Kagera ambapo husafirishwa kwa njia ya meli,” anafananua msafirishaji  huyo.

Zaidi, Bwana Kalinga, ambae pia ni mfanyabiasha wa bidhaa za chakula katika soko hilo, anaongezea kuwa ,kwa aonavyo yeye, hali hiyo pia haitoathiri bei za vyakula. “Bidhaa za vyakula haziwezi panda bei  kwa sababu kipindi hichi ni cha mavuno,” anasema.

Bwana kalinga ameendelea kusema kuwa kwa sasa bei za mchele, kwa mfano, zimeshuka toka kiasi cha TSH 2000 kwa KG moja na kuuzwa kati ya TSH 1700 na 1800; sababu kuwa msimu huu ni wa mavuno kutakuwa na mchele mwingi sokoni, bei ya mchele haitoweza kupanda. 

“ Kama unavyojua kama bei imeshuka huko tunapochukua kwa mkulima hiyo haiwezi kutufanya kupandisha bei za vyakula, ukiangalia maharagwe na mahindi tunanunua Bukoba na tunasafirisha kwa meli lakini katika kusafirisha mzigo mkubwa kama tunaosafirisha melini wala nauli yake haipandi kwa hiyo hatuwezi kupandisha bei” anasisitiza .

Dr. Odass Bilame, mchumi kutoka chuo kikuu cha Mt. Augustine Tanzania (SAUT), amesema kuwa licha ya kuwa kwa sasa ni msimu wa mavuno, baada ya msimu huu kupita kwa kiasi fulani gharama za bei za vyakula zitapanda kutokana na upandaji huu wa nauli kuathiri gharama za usafirishaji. 

Pia, Dr. Bilame anaongezea kuwa mfumuko wa bei utaathiri sana wananchi ambao kipato chao ni cha chini; tabaka kati ya masikini na matajiri litaongezeka. “Mishahara, kwa mafano, wanayopewa walimu ni midogo ukilinganisha na ya mawaziri. Hivyo, kupanda kwa bei za nauli kutaathiri sana gharama za maisha yao na hivyo, kushindwa kutimiza malengo yao ya kuwa na maisha bora,”anasema Dr. Bilame.

Hata hivyo, Dr. Bilame anatoa angalizo kwa serikali kuwa inatakiwa kuangalia mfumuko wa bei wakati ikifanya maamuzi ya bei za vitu kupanda, kama iilivyopandisha bei za nauli kwani mfumuko wa bei unaathiri fursa endelevu za kiuchumi kwa wananchi na hivyo, kuikosesha nchi yetu kushinda tuzo ya utawala na maendeleo ya uchumi katika nchi za Afrika. 

Pia, anaishauri serikali kuwa na mpango maalumu wa kuwashirikisha wadau mbalimbali kabla ya kufanya maamuzi ya kupandisha nauli badala ya kufanya maamuzi hayo pekee yao.
Mwisho, Dr. Bilame aliitaka serikali kupunguza kiwango cha kodi kwenye mafuta kwani ndio sababu kubwa ya nauli kupanda. 

kwa upande wa wasafirishaji, Dr. Bilame anawataka waangalie uwezekano wa kununua vyombo vya usafiri vilivyovipya ili kuondokana na gharama za kununua vipuri mara kwa mara kwa ajili ya vyombo hivyo ambavyo ni chakavu. 

Kupanda kwa bei za nauli kulitangazwa mwanzoni mwa mwezi huu na SUMATRA, chombo chenye mamlaka ya kisheria kufanya mapitio ya bei za nauli; bei hizo zimekwishaanza kazi rasmi tangu jana tarehe 12/04/2013, licha ya wasiwasi unaoonekana katika jamii juu ya kupanda kwa gharama za maisha na hivyo, kufanya maisha kuwa magumu zaidi kwa baadhi ya watu, hasa wenye kipato cha chini.


0 comments:

SUBSCRIBE- Andika email yako hapa utumiwe habari mpya

Enter your email address:

Delivered by FeedBurner

  © Blogger templates 'Neuronic' by Ourblogtemplates.com 2008 modified by Subi nukta77

Go Back to TOP