Pekua/search

Wednesday, May 22, 2013

NATAMANI SANA

Natamani sana
Tamaa yangu ni kubwa
Kubwa kuliko niwezavyo sema
Kubwa sana hata siwezi maliza

Tazama watu wa mtwara
Wamepigwa mikwara
Wamepigwa mabomu
Kisa gesi 'yao'

Je ni yao
Yao peke yao
Iwafae wao
Kwa manufaa yao

Ni ya nani?
Je ya kiongozi nani?
Anamiliki nani?
Kwa manufaa ya nani?

Nachelea nisiwe miongoni mwao
Hao wawasemao
Wana wa Mtwara kuwa wamepoka gesi

Nisiwe miongoni mwa wanaolaumu
Eti mataifa ya nje yanaleta chokochoko,
Chokochoko tumeileta sisi
Kwa kutokujua haki za wazawa

Wanayo haki, haki ya kudai pato la gesi,
Wanayo haki ,haki ya kumiliki gesi
Hata kama sheria inasema madini ni ya UMMA,
Wao sio umma au umma wa nani?

Nani atasimama ataonesha usawa katika utajiri wa madini tuliobarikiwa nao
Nani atasimama atasema kuwa eti tumefaidika,,kwa kujengewa shule? Vyoo?
 Kwani TOFARI moja la DHAHABU lajenga VYOO, SHULE, ZAHANATI NGAPI?
Twahitaji MATOFARI mangapi ya TANZANITE ili tujenge barabara?

Wanayo haki,
Ya kutaka kuona namna watakavyofaidika,
Sio kuwapa ahadi
Zile za kwenye majukwaa.

Ifike mahali watu waoneshwe
Wapate kushika,
Hata Tomaso alikataa
Mpaka akatomasa

Vikionekana
Havibishiwi
Vikishikwa
Havikataliwi.

Pengine ni namna tu
Ya walivyodai
Wafanyeje
Kama mahakama ni sehemu ya dola

Wanayo kumbukumbu
Walimu walivyokomeshwa kugoma
Maana mahakama iligoma
Kuwaacha walimu wagome.

Wafanyeje,
WANA wa SIASA si wana WAO tena
Maana wao ni TAIFA teule
Lisiloguswa?

Wana wa SIASA,
Wana HISA
Wanafanya VISA
Utajiri waufaidi wao

Hawakuwa na namna nyingine
Pole wahanga wote
Hamtakwenda bure
Maana mfumo umewapoteza

Guebuza zamani alisema,,if we must die, let us die not like hogs
Hamjafa bure,
Mmefia 'a good cause',
Mungu awape subira, enyi wana wa MTWARA
Itapita hii MIKWARA,
MTASIKIWA.

Tamaa yangu ni kubwa
Kuona mali zetu twazifaidi
Sio kama KIWIRA COAL MINE
Mgodi umefungwa, Kisa ni nini? Waulize wana wa SIASA.

NATAMANI SANA,

WOTE KWA UMOJA TUGOME, TUDAI DHAHABU YETU, TWIGA WETU, NYATI WETU, FALU WETU, TANZANITE YETU, UTAIFA WETU,,,,NA MWISHO UTU WETU,,,


natamani sana,,,,

1 comments:

Gwanka May 24, 2013 at 11:39 AM  

Mawazo na hoja kuntu. Mwenye ufahamu na aelewe.

SUBSCRIBE- Andika email yako hapa utumiwe habari mpya

Enter your email address:

Delivered by FeedBurner

  © Blogger templates 'Neuronic' by Ourblogtemplates.com 2008 modified by Subi nukta77

Go Back to TOP