Pekua/search

Tuesday, July 10, 2012

Mgomo wa madaktari ni darasa- Wako wapi Wanafunzi?


Udhaifu wa hoja si hoja, hoja ni tafakuri yake

 
Na Adam Gwankaja.
Makala haya yalichapishwa mwezi Februari kwenye safu ya Hoja dhaifu gazeti la AFRIKA LEO. Hata hivyo mgomo umekuwa nasi tena sasa kwa mara nyingine, hoja dhaifu katika makala haya bado zina mashiko, ni vema kuzirejea. Kama kawaida udhaifu wa hoja si hoja hoja ni tafakuri yake. Tuendelee kutafakari.
 
Mgomo wa madaktari umetokea na madhila yake tumeyapata. Umekwisha rasmi kuelekea mwishoni wa wiki iliyopita. Inaelekea hata madaktari wenyewe hawakuupenda, ila ndiyo hivyo umetokea. Hatuwezi kurushia siku nyuma kuuzuia usitokee, tusipate maumivu yaliyopatikana, lakini tunaweza kuutumia kuzuia uwekano wa kutokea tena. Tunaweza kujifunza tukitaka.

Tunapofurahia kwisha kwa mgomo wa wataalamu hawa huku tukigugumia maumivu tuliyoachiwa, ni vema kutafakari hoja hii dhaifu ya mambo tunayojifunza kutokana na mgomo huu.

Naam mgomo huu umekuwa darasa maridhawa kwa kila mwenye pumzi nchini. Ni darasa mwanana tena ambalo ada yake ni kubwa, na tumeilipa japo stakabadhi hatukupewa wala hatukudai.

Serikali yetu, uongozi wetu na watawala wetu hapana shaka wamejifunza kuwa mabavu hayalipi. Wamejifunza kuwa uziwi wa kuigiza hausadii maana hivi sasa ndiyo wenye kubeba lawama nambari wani kwa yote machungu yaliyosababishwa na mgomo huu. Serikali ikaweka kichwa ngumu kusikiliza kero za mabingwa hawa muhimu, mwishowe ustahimilivu wao wa kawaida ukawashinda wakalazimika kuacha kufanya kazi kuishinikiza serikali kusikiliza. Viongozi wakuu wa utumishi wa umma hapana shaka wamejifunza kuwa ni muhimu kuwasimamia kwa karibu watumishi walioko chini yao.

Warasimu watakuwa wametambua kuwa jeuri halipi. Kusimamishwa kazi Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii Blandina Nyoni na Mganga Mkuu wa serikali Deo Mtasiwa ni salamu na ujumbe muhimu kwa warasimu wote kwamba cheo ni dhamana. Ni ushuhuda muafaka kwamba hakuna mwenye mamlaka yasiyo ukomo.

Inakuwaje katika mfumo mzuri wa uendeshaji taasisi za umma na utawala, Waziri Mkuu asijulishwe matatizo makubwa yanaikumba taasisi nyeti kama Hospitali ya Taifa ya Muhimbili hadi Madaktari Mabingwa wagome ndipo aambiwe? Warasimu hawakuwajibika. Watakuwa wamejifunza na watatimiza wajibu wao pasipo kuendeleza porojo kuwa wanaingiliwa na wanasiasa.

Madaktari na watumishi wengine wa umma kama vile walimu hapana shaka mgomo huu umewapelekea salamu kwamba licha ya maumivu kama kipigo na matusi, kebehi na kudharauliwa, kusimamia haki zao, umoja na kujipanga hulipa.

Licha ya madhila ya siku hizi takribani 17 za mgogoro, kusimama kwao kidete, madaktari wameweza kulazimisha serikali si kuwasikiliza tu bali kuanza kuchukua hatua za kutatua kero zao nyingi zikiwa za msingi katika utoaji wao huduma.

Kisingizio cha kawaida cha serikali ni bajeti finyu. Sasa mbona baada ya kubanwa imeweza kupandisha posho za madaktari kutoka shilingi 10,000 hadi kati ya shilingi 25,000 na 35,000 tena ndani ya bajeti ya mwaka huu wa fedha? Somo la vipaumbele hapa linahusika sana. Serikali isipotaka kuweka vipaumbele kwa masuala ya msingi, basi ilazimishwe kufanya hivyo kwa maslahi ya taifa kama ilivyotokea katika mgogoro huu.

Na kwa watanzania wote pamoja na wanaharakati somo liko wazi kuwa kuchekea udhalimu hailipi. Tunajifunza kuwa tukisimama pamoja na kusema hapana kwa udhalimu na manyanyaso basi vitakoma. Nguvu iliyoongezwa na maandamano ya wanaharakati kuishinikiza serikali kusikiliza na kuyafanyia kazi madai ya madaktari haiwezi kupuuza katika kutufikisha tulipofikia ambapo madaktari wamekubali kurejea kazini.

Na kwa upande wa pili tamko la msisitizo la madaktari kutaka wanaharakati waliotiwa msambweni kwa kutumia haki yao ya msingi nay a kikatiba kuandamana kueleza hisia zao waachiwe pia haliwezi kupuuzwa tamko hilo katika kuachiwa kwa watanzania hao, raia wema.

Migogoro ya aina hii inayohusisha kudai haki za kundi fulani la jamii ni kama mtego wa panya ambamo wanaingia waliokuwemo na wasiokuwemo. Sote tunapaswa kuwa na nia moja. Tuendelee jufunza wingi wa elimu iliyomo kwenye matukio ya aina hii, itusaidie kuboresha maisha yetu nchini. Udhaifu wa hoja si hoja hija fakuri yake. Tuonane juma lijalo. 


0 comments:

SUBSCRIBE- Andika email yako hapa utumiwe habari mpya

Enter your email address:

Delivered by FeedBurner

  © Blogger templates 'Neuronic' by Ourblogtemplates.com 2008 modified by Subi nukta77

Go Back to TOP